Habari Zetu :

Home » , » HOJA YA MBATIA YAZIKWA

HOJA YA MBATIA YAZIKWA

Written By Unknown on Friday, February 8, 2013 | 11:28 AM



SUALA la mitalaa ya elimu nchini limeibuka tena bungeni jana baada ya mtoa hoja, James Mbatia kusema hakubaliani na mitalaa iliyowasilishwa kwa Spika kama kielelezo cha kuwepo kwake.
Juzi Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa aliwasilisha mitalaa ya elimu kama alivyodai Mbatia baada ya kuwasilisha hoja binafsi iliyozungumzia udhaifu wa elimu.
Hata hivyo, kabla ya kuthibitishwa na Bunge, Naibu Spika, Job Ndugai aliunda kamati kuichunguza mitalaa hiyo kuangalia uhalali wake.
Kamati hiyo iliyopewa kazi ya siku moja, ilikuwa chini ya mwenyekiti wake, Magreth Sitta pamoja na Mbatia mwenyewe. Wajumbe wengine wa kamati ni Benadetha Mshashu, Abdul Jabil, Khalifa Khalifa, Yahaya Kassim Issa na Israel Natse.
Akiwasilisha taarifa ya kamati bungeni jana, Spika wa Bunge, Anna Makinda alisema:
“Baada ya Serikali kuwasilisha mitalaa ili kujiridhisha, iliunda kamati kuchunguza ukweli wa mitalaa hiyo.
“Baada ya kukabidhiwa nyaraka mbalimbali kuhusiana na hilo, kamati iliwasilisha taarifa yake ya kuthibitisha kuwa mitalaa hiyo ilikuwa halali na sahihi na ninaagiza igawiwe kwa wabunge,” alisema Makinda kabla ya kuahirisha Bunge.
Baada ya hoja ya Spika, Mbatia aliomba mwongozo wa Spika na alipopewa nafasi alisema: “Kwa mujibu wa Kanuni 37 (4), baada ya hati kuwasilishwa, Mwanasheria Mkuu ana wajibu wa kuwasilisha taarifa ya kutaka hoja ijadiliwe.
Mbatia atoa ufafanuzi
Akizungumza na waandishi wa habari jana baada ya kutoka katika Ukumbi wa Bunge, Mbatia alisema kuwa hakubaliani na mitalaa iliyowasilishwa ambayo ni ya elimu ya awali, msingi na sekondari.
Alisema kilichowasilishwa siyo alichokidai bungeni, mtalaa alioudai ulikuwa wa mwaka 1997 hadi mwaka 2005 wakati uliowasilishwa ni wa mwaka 1998 hadi 2008 ambao unasema ni kwa ajili ya Tanzania Bara.
“Huwezi kusema Mtalaa wa Elimu ya Sekondari ni wa Tanzania wakati huu uliopo unaonyesha ni wa Tanzania Bara wakati hata mtihani unaofanyika wa darasa la saba ni wa Tanzania.
“Kasoro nyingine ni kwamba katika vitabu vya mwongozo inatakiwa kuwa na Alama Ubora (ISBN) kwa kuidhinishwa na Bodi ya Maktaba, sasa mtalaa wa jana hauna hayo yote.”
Kasoro ya tatu, Mbatia alisema alikataa muhtasari kwa kuwa haukuwa na saini ya Kamishna wa Elimu.
Alisema kuwa bado anasimamia hoja yake kuwa hakuna mitalaa ya elimu Tanzania na atasimamia hapo na atamwomba Spika suala hilo lijadiliwe na Wabunge wote kwa masilahi ya taifa, kwani mtalaa wa taifa hauwezi kutolewa kwa waraka.
Kawambwa azungumza
Akijibu hoja za Mbatia, Waziri wa Elimu, Shukuru Kawambwa alisema; Suala la kuweka alama ya ubora, halina mashiko kwa kuwa hutolewa kwa machapisho ya ndani na nje ya nchi.
Hata hivyo, alisema suala hilo linasimamiwa na maktaba kuu.
“Mimi ninachotaka kusema, mitalaa iliyowasilishwa ndiyo hiyo na Kamati imemsaidia Spika kumweleza na kumhakikishia hili, nimesikitika sana na hoja zake kuwa zinataka kupotosha na naweza kusema vielelezo alivyotoa ni feki.
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

PROFESSIONAL BLOG DESIGNERS

PROFESSIONAL BLOG DESIGNERS

IDADI YA WATU

BLOG ARCHIVE

DROP YOUR COMMENTS HERE

 
Designed by : Bongo Blogs Designers | Bloggerized by | Tryphone Chasama Jr
Contacts: 0719 625003 / 0765 860437Welcome
Copyright © 2011. SNOUT HOT NEWZ - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template